Kenya yafikiria sheria kupambana na udanganyifu katika mitihani ya sekondari

Na Bosire Boniface, Wajir

Mei 15, 2012

  • + Toa maoni sasa
  • Chapisha
  • Panga upya Punguza Ongeza

Baraza la Mitihani la Kenya (KNEC) limetunga rasimu mpya ya sheria ambayo itafanya udanganyifu kwenye mitihani ya taifa kuwa uhalifu, baada ya tuhuma za udanganyifu mkubwa uliosababisha kufutwa kwa matokeo ya karibuni wanafunzi 3,000 mwaka huu.

  • Wanafunzi wakiandamana katika mitaa ya Garissa kufuatia kufutwa kwa matokeo ya mtihani wa sekondari mwezi Machi. [Bosire Boniface/Sabahi]

    Wanafunzi wakiandamana katika mitaa ya Garissa kufuatia kufutwa kwa matokeo ya mtihani wa sekondari mwezi Machi. [Bosire Boniface/Sabahi]

  • Walimu wakishiriki katika kikao cha uchunguzi wa kufutwa kwa mitihani ya sekondari mjini Garissa tarehe 13 Aprili. [Bosire Boniface/Sabahi]

    Walimu wakishiriki katika kikao cha uchunguzi wa kufutwa kwa mitihani ya sekondari mjini Garissa tarehe 13 Aprili. [Bosire Boniface/Sabahi]

Afisa Mtendaji Mkuu wa KNEC, Paul Wasanga, alisema Waziri wa Elimu Mutula Kilonzo aliuwasilisha msaada huo bungeni mwezi Aprili na wabunge wanatarajiwa kujadili marekebisho yoyote na kuupigia kura kuwa sheria mwaka huu.

“Hadi sasa serikali haijawahi kumshitaki hata mtu mmoja kwa udanganyifu kwenye mitihani ya taifa. Tabia hii imekuwa ikiongezeka kwa miaka mitano iliyopita kwa hivyo sasa tunakuja na hatua kali,” Wasanga aliiambia Sabahi

Wanafunzi wa Kenya wanatakiwa kufanya mtihani wa taifa wa Cheti cha Elimu ya Sekondari mwishoni mwa mwaka wao wanne wa sekondari ili kupata vyeti vya kuhitimu, ambapo bila ya vyeti hivyo hawawezi kuomba kazi au kuendelea na elimu ya chuo kikuu.

Chini ya sheria hiyo inayopendekezwa sasa, wadanganyifu watazuiwa kufanya mitihani kwa kipindi cha hadi miaka mitatu. Wao na washirika wao wanaweza kufungwa hadi miaka 10 jela na faini ya shilingi milioni 2 za Kenya (dola 24,000), alisema Wasanga.

Watu wanaovujisha mitihani au sehemu ya karatasi za mitihani na vifaa vyake atakabiliwa na adhabu ya hadi miaka mitano jela na faini ya hadi shilingi milioni 1 (dola 12,000). Mtu yeyote atakayegunduliwa wakati au kabla ya mtihani na sehemu ya mtihani atashitakiwa.

Pamoja na hayo, wafanyaji mitihani wanaojisajili kwa majina bandia na wale waliowaruhusu wanafunzi kufanya mitihani kwa majina yao wataweza kukabiliwa na kifungo cha hadi miaka miwili jela na faini ya shilingi milioni 1.

“Tunatarajia kwamba sheria hii itapitishwa kwa haraka mwaka huu kudhibiti wadanganyifu na washirika wao,” alisema Wasanga.

Mwezi Februari, KNEC ilifuta matokea ya wanafunzi 2,927 kwa sababu ya kukiukwa kwa taratibu na tuhuma za udanganyifu mkubwa. Kwa mujibu wa baraza hilo, kati yao matukio 1,694 ya uvunjaji wa taratibu za mitihani yaliyotokea kwenye Jimbo la Kaskazini Mashariki.

Ushirikiano kati ya wanafunzi, walimu na watu wengine uliwezesha udanganyifu na uingizaji wa visaidizi vya mitihani katika vyumba vya mitihani vilikuwa chanzo cha tatizo, alisema Wasanga. Alisema ukiukwaji wa taratibu ulionekana wakati wa mitihani na wasimamizi.

Wanafunzi ambao mitihani yao imefutwa hawataweza kuendelea mbali hadi alama zao zitakapopatikana kihalali, alisema.

Mohamed Bunow Korane, mtafiti katika Jihan Foundation, ambayo inafadhili elimu kwa wasichana mjini Garissa, alisema mengi zaidi yanahitaji kufanywa kuhakikisha kuwa jimbo hilo halikabiliwi tena na ufutaji mkubwa wa matokeo ya mitihani, ikiwemo kutoa vifaa zaidi kwa shule.

Alisema vifaa visivyofaa katika skuli nyingi kwenye mkoa huo husababisha wanafunzi kutumia pamoja vifaa vya maabara hata wakati wa mitihani ya taifa.

“Mitihani ya sayansi kwa kawaida inafanyika kwenye maabara za shule na wasimamizi wa mitihani wanaona wanafunzi wakitumia vifaa pamoja kwenye maabara na kuhitimisha ni mpango wa kuwasaidia wanafunzi kudanganya,” Korane aliiambia Sabahi.

Kufutwa kwa mitihani kulichochea maandamano na vikao vya kijamii katika mkoa huo.

Sasa wanafunzi wanasubiri matokeo ya uchunguzi unaoendelea kuhusu matokeo ya mitihani ya taifa kutoka kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge juu ya Elimu. Mwenyekiti wa Kamati hiyo, David Koech, aliiambia Sabahi kwamba kamati yake bado inakusanya ripoti na itahakiki ugunduzi na mapendekezo yake bungeni hivi karibuni.

Uchunguzi huo uliagizwa baada ya viongozi waliochaguliwa kuwakilisha jimbo hilo wakiongozwa na mbunge wa Dujis, Aden Bare Duale, kulalamikia ufutwaji wa matokeo na kupeleka hoja bungeni ya kutaka bunge liuhakiki mtihani upya. Spika Kenneth Marende aliagiza uchunguzi huo hapo mwezi Aprili.

Mohammed Affey, mteule wa chama Orange Democratic Movement katika moja ya viti 12 vya ubunge vitakavyojazwa kwa uteuzi wa chama, aliiambia Sabahi kwamba udanganyifu unaweza kutokea, lakini akashuku uhakika wa ugunduzi wa KNEC.

Pia wanafunzi, walimu na wazazi walisema walishtushwa kwamba mkoa wao ulivunja rikodi ya idadi kubwa ya vitendo vya uvunjifu wa taratibu mwaka jana, na kuzua masuala dhidi ya ripoti ya ugunduzi wa KNEC katika kikao na kamati ya Bunge mjini Garissa hapo tarehe 13 Aprili.

Hussein Abdi Muhumed, mwanafunzi mwenye umri wa miaka 17 kutoka Garissa ambaye matokeo yake ya mtihani yalifutwa, amesema jambo hilo limemuathiri sana. Ufutwaji wa matokeo yake, alisema, unamaanisha hawezi kuendelea kwenda chuo kikuu au kutafuta kazi.

“Baada ya matokeo yangu kufutwa, nilijihisi nimeangamizwa”, aliiambia kamati ya Bunge katika kikao chake kwenye ukumbi wa Boys Town Secondary School.

Mzazi Adan Ibrahim Ahmed aliiambia kamati hiyo kwamba mkoa haujawahi kufanya vyema kwenye mitihani ya taifa kwa miaka 40 sasa na akawataka maafisa kuipa alama tena mitihani iliyofutwa.

Unaonaje kuhusu makala hii? (Jumla ya Kura 7)

Dislike_icon(2)

(Sera za kutoa Maoni) *Inaonesha Maeneo yanayohitaji

Habari Mpya kabisa

Katika Mwangaza

Jisajili

Kura

Je, unadhania kupigwa marufuku kwa hotuba ya chuki na Tanzania kutakomesha mashambulizi dhidi ya makanisa na misikiti?

Angalia matokeo

Nyenzo